Latest in Tech

MFAHAMU VEMA MAREHEMU KUCY KIBAKI

lucy kibaki
Kwa zaidi ya miongoni miwili Kenya ilikuwa inahitaji mwanamke wa kwanza.

Na ilipofikia mwaka 2002,Wapiga kura walimuunga mkono Mwai Kibaki na kwa bahati nzuri akatangazwa kuwa rais huku mkewe akiwa mke wa kwanza.

Hatua hiyo ilimaliza utawala wa aliyekuwa rais Daniel Moi ambaye aliliongoza taifa hilo kwa miaka 24 wakati ambapo mkewe hakuonekana hadharani.

Na alipokula kiapo Rais Kibaki Mkewe mama Lucy Kibaki alikuwa ametulia kando yake akiwa amevalia rinda lenye mtindo wa Kiafrika lenye rangi nyeupe na bluu.

Lakini baada ya siku nne pekee Bi Lucy Kibaki aliwashambulia wajumbe wa mataifa ya kigeni,waandishi na maafisa wa polisi ambao anahisi hawakumuheshimu.

Hatua hiyo ilizua wasiwasi mkubwa miongoni mwa Wakenya wa iwapo rais kibaki alikuwa ameshindwa kuongoza familia yake.

Kisa cha kwanza ni pale Bi Lucy Kibaki alipovamia nyumba ya Jirani yake Mkurugenzi wa benki ya dunia tawi la Kenya na kumtaka kupunguza sauti ya muziki katika sherehe ya kukamilika kwa uongozi wake nchini Kenya.

Kisa hicho kilitokea wakati ambapo Kenya ilikuwa ikitafuta kuimarisha uhusiano wake na Benki ya Dunia ambayo ilikuwa imekosoa Kenya kwa kuongezeka kwa Ufisadi.

Na siku iliofuatia Bi Kibaki alienda hadi katika kituo cha polisi akiwa amevalia kaptula-ikionekana na Wakenya wengi kama isio na heshima kwa mwanamke wa Kiafrika, na kutaka bwana Diop na wageni wake wakamatwe kwa kuharibu amani.

Na Jumatatu iliofuata alivamia afisi za kituo cha habari cha Nation na walinzi wake na kutaka ripota aliyeandika kuhusu kuingia kwake katika nyumba ya Diop akamatwe.

Alimchapa kofi mpiga picha Clifford Derrick ambaye alikuwa akichukua kanda ya video na kukataa kutoka katika afisi hiyo hadi saa kumi na moja asubuhi.

Siku ya Jumanne habari hiyo ilikuwa kichwa cha habari cha magazeti yote huku picha za kukasirika kwake zikitawala runinga zote.

Yote haya yalikuwa kinyume na mwanamke aliyezaliwa 1940 kutoka kwa familia yenye dini katika jimbo la Mount Kenya.

Marafiki wa karibu wa familia yake walizungumza kuhusu mwanamke aliyekuwa na haya na asiyezungumza sana ambaye alifanya vyema shuleni na kuwa mwanamke wa kwanza wa Kiafrika kufunza katika katika taasisi ya walimu.

Lucy Kibaki alikutana na Kibaki ambaye alikuwa amewacha kazi ya ualimu katika chuo cha Makerere nchini Uganda mwaka 1960 na mapenzi yao yakasababisha ndoa iliochukuwa miaka 35 na kuzaa watoto watano.

Kama mke wa mwanasiasa ,Lucy Kibaki alisalia na Kibaki huku Kibaki akipanda kutoka Mbunge wa kawaida hadi kuwa waziri na baadaye makamu wa rais chini ya Moi na hatimaye rais wa Kenya 2002.

Tangu wakati huo wote, ilikuwa wazi kwamba Bi Lucy hakuwa mke wa kwanza wa kawaida tu.

Miezi kadhaa baada ya mumewe kutangazwa kuwa rais ,aliripotiwa kuifunga baa moja ndani ya ikulu ya rais ambayo ilikuwa ukumbi wa mawaziri pamoja na wandani wa karibu wa rais.

Washauri wa mawaziri na wale wa rais ambao walikosana naye walitakiwa kuondoka katika jengo hilo mara moja.

Katika kisa kimoja,mgogoro kati yake na aliyekuwa katibu wa rais Kibaki ulipelekea katibu huyo kufurushwa katika ikulu ya rais.

Mwaka 2003,alisusia sherehe ya kuaga mwaka na kuingia mwaka mpya baada ya aliyekuwa makamu wa rais Moody Awori kumtaja mkewe wa pili swala alilolichukulia kama matusi.

Ni wakati huo ambapo Wakenya waligundua kwamba hawakumpata mke wa rais baada ya miaka 24 pekee bali walikuwa na wake wawili akiwemo mwanamke aliyejulikana kama Mary Wambui ambaye amekuwa rafiki wa Kibaki kwa miaka 30 na kwamba amekuwa akipokea usalama kutoka kwa serikali.

Lucy Kibaki vilevile alipendwa na wengi nchini kwa kampenni yake dhidi ya Ugonjwa wa ukimwi pamoja na ukeketaji wa wanawake.

Ijapokuwa Wakenya wengi walimpenda kwa dhati ,mapenzi yao kwake sasa yamekwisha.Ni wakati wa kufikiria jukumu la mke wa rais? Je,wanachangia vipi katika maendeleo ya taifa.

Je, unadhani wake za marais wa Afrika wana jukumu gani? Tuambie katika kiwango cha moja hadi kumi unamweka wapi mke wa rais wa taifa lako?

Share this:

Post a Comment

 
Copyright © bakinamimi. Designed by OddThemes & VineThemes