Donald Trump ameshinda mchujo wa
kuteua mgombea urais wa chama cha Republican katika majimbo matano ya
Marekani yaliyopiga kura Jumanne.
Baada ya matokeo kubainika, Bw Trump alijitangaza kuwa “mgombea mteule” wa Republican.
Ushindi wake Connecticut, Delaware, Maryland, Pennsylvania na Rhode Island unamfanya kukaribia sana kutimiza idadi ya wajumbe inayohitajika kumhakikishia ushindi kabla ya kuandaliwa kwa mkutano mkuu wa chama hicho wa kuidhinisha mgombea Julai.
Upande wa Democratic, Bi Clinton amenyimwa ushindi kamili na Bernie Sanders ambaye ameshinda katika jimbo la Rhode Island.
Bw Sanders ameaoa kuendelea na mchujo.
“Sisi tunaamini katika wema wa watu wetu na ukuu wa taifa letu,” alisema.
Naye Bw Trump aliwaambia wafuasi wake New York kwamba hatabadilisha sera zake iwapo atachaguliwa kuwa rais.
"Sibadiliki,” alisema. “Mnafahamu kwamba nilisomea shule bora zaidi. Mimi ni mtu mwerevu sana. Nitaiwakilisha nchi hii kwa heshima na vyema sana.
"Lakini sitaki kubadilisha sifa zangu binafsi. Mnajua, ndizo zilizonifikisha hapa.”
Wapinzani wake, Ted Cruz na John Kasich, tayari wameanza kuangazia majimbo yajayo, wakiungana kusaidiana kushinda majimbo ya Indiana, Oregon na New Mexico.
Bw Trump ameshutumu ushirika wao akisema ni ishara ya kukata tamaa.
Post a Comment