Latest in Tech

MUIGIZAJI MCHEKESHAJI KINYAMBE AFARIKI DUNIA

Mchekeshaji maarufu nchini Tanzania kutoka katika Kundi la Vituko Show, Mohammed Abdallah ‘Kinyambe’ amefariki dunia Jumatano hii baada ya kusumbuliwa kwa muda mrefu na uvimbe tumboni.
Taarifa za kifo chake zilianza kuzagaa jana katika mitandao ya kijamii baada ya wasanii wa filamu kuanza kupost picha mbalimbali huku wakiandika RIP Kinyambe.

Akizungumza na Bongo5 Alhamisi hii mmoja kati ya wasanii wanaounda Chama Cha Wasanii Wachekeshaji Tanzania, Mkono Mkonole, amesema Kinyambe amefariki jana akiwa mkoani Mbeya.

“Kinyambe alikuwa anasumbuliwa na uvimbe tumboni kwa muda mrefu, ila jana ndo amefariki akiwa mkoani Mbeya, katika hospitali ya mkoa wa Mbeya,” alisema Mkonole.

Kuhusu taratibu za mazishi, Mkonole amesema bado hawajapanga kwani taarifa za kifo chake wamezipokea jana usiku.

“Kusema kweli bado hatujapanga kuhusu mazishi, lakini sasa hivi tunawasiliana na ndugu zake ili kujua taratibu za mazishi na zikamilika tutaweka wazi,” alisema Mkono.

Kinyambe atakumbukwa kwa uwezo wake wa kuigiza, hasa hasa jinsi anavyoongea pamoja na mtindo wake wa pekee wa kugeuza macho.

Baada ya taarifa hizo, wasanii mbalimbali wa filamu na muziki walishare ya moyoni jinsi walivyozipokea taarifa hizo za kusikitisha.

Share this:

Post a Comment

 
Copyright © bakinamimi. Designed by OddThemes & VineThemes